Saturday 20 July 2013

Hakimu Mkazi Kisutu

 
 
 
 
 
 
 
 
 
WAKAZI wawili wa Dar es Salaam, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa ajili ya hapo baadae kuja kuunganishwa katika kesi ya wizi wa Paspoti 26 inayomkabili Msainii wa Muziki wa asili, Chingwele Che Mundugwao (pichani) na wenzake wanne.
Wakili wa serikali Aidah Kisumo mbele Hakimu Mkazi Sundi Fimbo aliwataja washitakiwa hao walifikishwa jana kwa mara ya kwanza mahakamani hapo wakikabiliwa na makosa yanayofanana ambayo yanamkabili Chemundugwao na wenzake ni Rajab Momba na Haji Mshamu.

Akiwasomea mashitaka Momba na Mshamu, Wakili Kisumo alidai kuwa tarehe isiyofahamika washitakiwa walikula njama ya kutenda kosa. Aidha tarehe tofauti Dar es Salaam, Momba aliiba hati ya kusafiria yenye namba AB 651926 mali ya serikali.

Alidai Momba, Mshamu na Iqbal wanadaiwa tarehe isiyofahamika Dar es Salaam, walighushi hati ya kusafiria yenye namba hiyo, kuonesha ni halali na imetolewa na Idara ya Uhamiaji ya Tanzania jambo ambalo si kweli.

Mbali na Che mundugwao washitakiwa hao wataunganishwa na Raia wa Uingereza Ahsan Iqbal au Ali Patel, Ofisa Ugavi wa Idara ya Uhamiaji Shemweta Kiluwasha, Injinia Keneth Pius wa Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji na mfanyabiashara Ally Jabir.

Hata hivyo washitakiwa hao walikana mashitaka na kurudishwa rumande kwa kuwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP),Dk.Eliezer Feleshi aliwasilisha hati ya kuwafungia dhamana washitakiwa hao wawili kama alivyofanya kwa kina Chemunduwao na wenzake na kwamba upelelezi bado haujakamilika na kesi itatajwa tena Julai 22, mwaka huu, ili waunganishwe na Chemundugwao ambapo kesi yao nayo imepangwa kuja kutajwa Julai 22 mwaka huu.
Juni 3 mwaka huu, Chemundugwao na wenzake walifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani hapo wakikabiliwa na makosa mbalimbali yakiwemo kosa la wizi wa paspoti 26, ambapo hata hivyo DPP aliwasilisha hati ya kuwafungia dhamana ambapo hadi sasa wapo gerezani.

No comments:

Post a Comment